Tuesday, December 26, 2017

RPC SHANNA: ATAKAEFUNGA BARABARA NA KUCHOMA MATAIRI MKESHA WA MWAKA MPYA KUKIONA.

Kamanda wa polisi mkoani Pwani (ACP) Jonathan Shanna ,ametoa onyo kwa watu wenye tabia ya kufunga barabara kwa kuchoma matairi katika mkesha wa mwaka mpya na kupelekea usumbufu kwa watuamiaji wengine wa barabara kuacha kufanya kitendo hicho .

Amesema atakaejaribu kuchoma moto matairi kwenye mkesha huo,jeshi la polisi mkoani hapo litamchukulia hatua kali ili iwe fundisho kwa wengine.
Akizungumza na waandishi wa habari kuhusiana na hali ya kiusalama
inavyoendelea hasa katika kipindi hiki cha kuelekea kwenye sikukuu ya mwisho wa mwaka ,kamanda Shanna alisema wanazidi kuimarisha doria katika pande zote za mkoa huo.
Alisema kipindi cha sikukuu ya x-mas hali ilikuwa shwarii hivyo wanaendelea na misako ya miguu kwa kushirikiana na vyombo vingine vya ulinzi na usalama na doria hizo zitakuwa mtaa kwa mtaa na nyumba kwa nyumba ili kuhakikisha watu waishi kwa amani .
Akielezea kuhusiana na hali ya uhalifu katika kipindi cha Januari hadi disemba mwaka huu ndani ya mkoa huo ,kamanda Shanna alisema wamefanikiwa kupunguza idadi ya makosa kwa kiwango kikubwa.
Kamanda huyo alisema,matukio ya makosa ya uvunjaji yamepungua kutoka 771 kipindi kama hicho 2016 na kufikia 233 mwaka huu ikiwa ni tofauti ya matukio 538.
Makosa mengine ni yale ya unyang’anyi wa kutumia silaha ambayo yamepungua kutoka 31 mwaka jana hadi nane kwa mwaka 2017  tofauti makosa 23.
“Unyang’anyi wa kutumia nguvu  yameripotiwa makosa 43 ,kipindi kilichopita ilikuwa 112 tofauti makosa 69,:;na mauaji makosa yaliyoripotiwa januari hadi disemba mwaka huu ni 34 ,mwaka uliopita ilikuwa 126  tofauti ni makosa 92.” alifafanua kamanda Shanna.
Aliwataka wananchi kutoa ushirikiano kwa jeshi hilo mara wanapotilia shaka kundi ama mtu ni mhalifu ,kwani kila mmoja ana wajibu wa kudhibiti vitendo vya uhalifu .
Kamanda Shanna ,alisema Pwani yenye utulivu,amani ,yenye kushikamana inawezekana endapo kila mmoja atatimiza wajibu wake.

No comments:

Post a Comment