Mbunge
 wa Singida Mashariki ambaye pia ni Rais wa Chama cha Wanasheria 
Tanganyika (TLS), Tundu Lissu  jana  aligoma kutoka katika chumba cha 
mahakama kufuatia kuwepo kwa tetesi kuwa kuna baadhi ya polisi wametumwa
 kumkamata kiongozi huyo. .
Lissu
 alifika mahakamani hapo jana asubuhi kwa ajili kusimamia kesi ya 
migogoro ya ndani ya Chama cha Walimu Tanzania (CWT) iliyokuwa 
ikisikilizwa na Hakimu Proches Mushi.
Katika
 kesi hiyo, Kamati ya Utendaji ya CWT wilaya imefungua kesi dhidi ya 
Katibu Mkuu wa CWT, Yahaya Msulwa wakimtuhumu kwa matumizi mabaya 
madaraka.
Hata
 hivyo wakijadili muda wa kurudi tena kwa kesi hiyo, Lissu ambaye pia ni
 Rais wa Chama cha Wanasheria Tanganyika, (TLS) alisema kuna polisi 
waliovalia kiraia waliokuwa wakimngojea nje ili wamkamate na 
kumsafirisha kwenda Dar es Salaam.
Habari
 za kutaka kukamatwa kwa Lissu zilisikika  asubuhi katika mitandao ya 
kijamii baada ya kutumiwa ujumbe kuwa kuna maaskari waliovalia kiraia 
wanataka kumkamata.
“Mheshimiwa
 naomba kesi hii isisomwe tarehe 23 kwa sababu sitakuwepo nchini, 
natarajia kwenda Uganda kwenye kikao cha vyama vya Afrika Mashariki vya 
mawakili,”alisema na kuongeza:
“Lakini
 pia nimepewa taarifa kuwa hapo nje kuna polisi wananisubiri nikitoka 
wanikamate na kunisafirisha kwenda Dar es Salaam hivyo huenda tarehe 
hiyo (Julai 23) nisiwe huru kuhudhuria kesi.”
Akijibu maombi hayo Mushi alisogeza kesi hiyo hadi Septemba 27-29 kwa ajili ya kuendelea na ushahidi.
Mara
 baada ya kesi kuahirishwa, Lissu akafanya mkutano na waandishi wa 
habari ndani ya ukumbi wa mahakama hiyo na kudai hatatoka mahakamani 
hapo ili aone kama polisi wana uwezo wa kuingia na kumkamata.
“Leo
 asubuhi nimepata taarifa kutoka Dar es Salaam kwa mama watoto wangu 
kwamba polisi walikuja nyumbani kwangu kunitafuta na wakaelezwa kwamba 
yuko Dodoma kwa muda wa siku tatu,” alisema.
“Baada
 ya hapo wasamaria wema walinitaarifu kuwa Jeshi la Polisi Dar es Salaam
 limewaomba wenzao wa Dodoma wanikamate pindi tu nitakapotoka hapa na 
kunirejesha Dar es Salaam.”
Alipoulizwa
 sababu inayofanya polisi watake kumkamata, Lissu amesema ni kutokana na
 maoni yake aliyoongea juzi ya kuukosoa uongozi wa Rais Magufuli.
“Rais
 Magufuli na chama chake wameshindwa siasa na wanachofanya sasa ni 
kutumia mabavu lakini wao kama Chadema kamwe hawataogopa wala kukaa 
kimya kwani kazi yao si kumsifia Rais bali ni kumkosoa anapofanya 
vibaya,”amesema.
Lissu
 ambaye pia ni Mbunge wa Singida Mashariki alisema hakuna sheria yoyote 
inayowaruhusu polisi kumkamata wakili akiwa katika shughuli zake 
mahakamani.
“Nakaa
 nione kama watavunja sheria ya kuja kunikamatia hapa hapa mahakamani. 
Nimeshazoea kukamatwa tangu mwaka huu uanze nimekamatwa mara nne,”alisema.
Baada
 ya kukaa mahakamani kwa saa nne, alifika Kamanda wa Polisi Mkoa wa 
Dodoma, Lazaro Mambosasa na kumweleza Lissu kwamba Jeshi la Polisi 
Dodoma halina taarifa yoyote wala mpango wowote wa kumkamata.
“Hatujapokea
 taarifa yoyote wala maelekezo yoyote ya kukukamata kutoka makao makuu. 
Hata ingekuwa hivyo tungeshakukamata kwa sababu muda wa mahakama 
umekwisha. Kwa sasa hivi yamebakia majengo tu kwa hiyo uwe huru uendelee
 na shughuli zako,” Mambosasa alimwambia mbunge huyo.
Baada ya Mambosasa kuondoka katika mahakama hiyo, Lissu naye aliondoka katika eneo hilo.
 

 
No comments:
Post a Comment