Wakati
 Kampuni ya Acacia ikisema imepoteza mapato ya Sh385 bilioni katika 
kipindi cha miezi sita kutokana na kuzuiwa kusafirisha mchanga wa madini
 nje, Rais John Magufuli ametishia kufunga migodi ya wawekezaji iwapo 
hawatajitokeza mapema katika mazungumzo.
Rais
 Magufuli amesema hayo takriban wiki moja baada ya kudokeza kuwa 
Serikali ingeanza mazungumzo “na waliokuwa wanatuibia” mapema wiki hii.
Jana,
 Rais Magufuli alisema Serikali haitasita kufunga migodi yote ya madini 
ambayo wamiliki walitakiwa kufanya mazungumzo na Serikali kuhusu ulipaji
 kodi.
 Akizungumza
 katika ziara yake mkoani Kigoma ambako alizindua Barabara ya 
Kibondo-Nyakanazi, Rais Magufuli alisema Taifa linapoteza fedha nyingi 
kutokana na upotevu wa madini.
“Ni
 matrilioni ya fedha ambayo yanapotea, na sasa hivi tumewaita tufanye 
mazungumzo lakini wakichelewachelewa nitafunga migodi yote,” alisema.
Alisema ni bora migodi hiyo ikakabidhiwa kwa Watanzania kuliko wawekezaji ambao hawalipi kodi.
Rais
 Magafuli alipiga marufuku usafirishaji wa mchanga huo nje ya nchi, na 
baadaye kuunda kamati mbili; moja ya kuchunguza kiwango cha madini 
kilichokuwa katika makontena 277 yaliyozuiwa Bandari ya Dar es Salaam na
 nyingine kuangalia athari za kiuchumi na kisheria tangu mchanga huo 
uanze kusafirishwa mwaka 1998.
Ripoti
 ya kamati ya kwanza ilisema kuwa Acacia, inayoendesha migodi ya 
Bulyanhulu na Buzwagi, haikusema ukweli kuhusu kiwango cha dhahabu, 
ikidai kuwa imebaini mchanga huo una madini hayo mara kumi ya kiwango 
kilichotangazwa na wawekezaji hao.
Ripoti
 ya kamati ya pili ilionyesha kuwa katika kipindi cha miaka 20, Serikali
 ilipoteza zaidi ya Sh108 trilioni na kwamba Acacia haijasajiliwa nchini
 na hivyo inafanya kazi kinyume cha sheria.
Hata
 hivyo, Acacia haijakubaliana na matokeo ya ripoti hizo, ikisema inataka
 uchunguzi wa kamati huru na kwamba kama matokeo hayo ni ya kweli, 
Tanzania ingekuwa moja ya nchi tatu zinazozalisha dhahabu kwa wingi 
duniani.
Jana,
 Acacia ilisema imepoteza Sh385 bilioni katika kipindi cha miezi sita. 
Acacia pia imesema endapo hali itaendelea kuwa hivyo, italazimika 
kuufunga mgodi wake wa Bulyanhulu na kusitisha mikataba ya ajira kwa 
wafanyakazi.
Hata
 hivyo, katika taarifa yake ya jana inayozungumzia kipindi cha Januari 
mpaka Juni, Acacia imesema  imepata changamoto kubwa katika utendaji 
wake nchini.
 “Nusu
 (ya kwanza), imetupa changamoto kubwa katika shughuli zetu Tanzania 
baada ya kuwekewa zuio la usafirishaji wa makinikia kuanzia Machi,” 
alisema Mkurugenzi Mtendaji wa Acacia, Brad Gordon. “Mapato yetu 
yameshuka mpaka dola 175 milioni za Kimarekani kutoka dola 318 milioni 
tulizotarajia.”
Licha
 ya kushindwa kuingiza Dola 175 milioni za Marekani (zaidi ya Sh385 
bilioni) zilizotarajiwa, Acacia inasema imelipa dola51 milioni za Kodi 
ya Ongezeko la Thamani (VAT), ambazo ni zaidi ya Sh112.2 bilioni.
Ili
 kulinda masilahi ya wanahisa wake, Acacia imewasilisha notisi kwa 
msuluhishi kwa ajili ya migodi ya Bulyanhulu na Buzwagi ambayo ndiyo 
inayozalisha mchanga wa madini kwa sasa.
Buzwagi
 imekuwa ikisafirisha mchanga huo kwenda nje ya nchi kwa ajili ya 
kuuyeyusha ili kupata mabaki ya dhahabu, shaba na fedha kutokana na 
teknolojia hiyo kutokuwapo mgodini.
Hatua
 ya kwanza ya kuchenjua dhahabu hufanyika mgodini na mchanga unaosalia 
ndio unaosafirishwa nje. Acacia imekuwa ikieleza kuwa mchanga huo una 
asilimia 0.02 ya dhahabu wakati shaba ni asilimia 10.
Acacia pia imekanusha taarifa ya kuwapo amri ya kutakiwa kuondoka nchini kwa mmoja wa wafanyakazi wake wa kigeni.
“Hatuna
 taarifa za kutolewa kwa amri hiyo kwa mfanyakazi wetu yeyote wa kigeni 
aliyepo Tanzania. Tunashirikiana vizuri na Serikali kwenye mazungumzo 
yanayoendelea na hakuna aliyekamatwa habari hiyo si sahihi,” inasema 
taarifa hiyo.
 

 
No comments:
Post a Comment