Mahakama ya Juu imefuta matokeo ya urais yaliyompa ushindi Rais Uhuru Kenyatta kuwa madarakani kwa muhula wa pili.
Mgombea
 wa Muungano wa Nasa, Raila Odinga alifungua kesi mahakamani kupinga 
matokeo ya uchaguzi huo uliofanyika Agosti 8, akisema ulitawaliwa na 
udanganyifu ikiwemo kuchezewa mitambo ya kujumlishia matokeo.
Katika
 uamuzi wake, Mahakama imesema uchaguzi huo ulikuwa na dosari nyingi, 
hivyo kukiuka misingi ya uchaguzi huru na wa haki kama ilivyoelekezwa 
katika Katiba ya nchi hiyo.
Hii
 ni mara ya kwanza katika historia ya Taifa hilo kwa Mahakama ya Juu 
kufuta matokeo ya uchaguzi na inaweka rekodi mpya katika historia ya 
uchaguzi barani Afrika ndani ya mfumo wa vyama vingi.
Katika
 uchaguzi uliopita, Odinga alienda mahakamani kupinga matokeo lakini 
Mahakama hiyo ilitupilia mbali hoja zake na kuridhia matokeo yaliyompa 
ushindi Rais Kenyatta.
Katika
 uchaguzi wa Agosti 8, Kenyatta alitangazwa mshindi kwa kupata kura 
8,203,290 sawa na asilimia 54.27, huku mpinzani wake Odinga akipata kura
 6,762,224 sawa na asilimia 44.74.
Kwa
 uamuzi uliotolewa na mahakama, uchaguzi mwingine unapaswa kufanyika 
katika kipindi cha siku 60. Iwapo ushindi wa Kenyatta ungeidhinishwa 
angepaswa kuapishwa Septemba 12.
Kumekuwa
 na shamrashamra katika mitaa mbalimbali ya Nairobi na Mombasa 
kushangilia uamuzi huo, huku Odinga akiwa na wanasiasa wenzake 
wamepongeza wakisema watatoa taarifa zaidi baadaye.
 

 
No comments:
Post a Comment