Saturday, September 2, 2017

Serikali yaongeza muda wa uhakiki wa Mashirika Yasiyo ya Kiserikali


Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto ambayo inajukumu la kusajili, kuratibu na kufuatilia uendeshaji wa shughuli za Mashirika Yasiyo ya Kiserikali nchini imeamua kuongeza muda wa siku 16 kwa Mashirika ambayo bado hayajahakiki  taarifa zake kwa Msajili wa Mashirikka yasiyo ya Kiserikali kukamilisha uhakiki huo.

Akizingumza na waandishi wa Habari Mjini Dodoma jana  Katibu Mkuu Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto anayeshughulikia Maendeleo ya Jamii Bibi Sihaba Nkinga alisema kuwa kumekuwa na mwitikio mkubwa wa Mashirika yasiyo ya kiserikali kuja kuandikisha taarifa za asasi zao katika vituo mbalimbali vya usajili vya kanda.

Bibi Sihaba aliongeza kuwa Serikali ina nia njema ya na siyo mbaya kama watu wanavyohisi katika utekelezaji wa zoezi hili la uhakiki linaloendelea nchi nzima katika vituo vya Kanda tano (5), na lengo ni la zoezi ni kutambua takwimu halisi ya Mashirika yanayofanya kazi ili kuweka utaratibu mzuri wa kutambua mchango wa kila asasi katika kuhudumia jamii katika nyanja mbalimbali.

“Niwaombee wadau wetu watumie muda huu tuliouongeza vizuri kwa kujitokeza kwa wingi kufanya uhakiki wa Mashirika yao na wale wenye changamoto tutawaelekeza namna bora ya kuzitatua,” alisema Bibi Sihaba.

Aidha Msajili wa Mashirika yasiyo ya kiserikali Bw. Marcel Katemba aliwahikikishia wadau wa mashirika yasiyo ya kiserikali nchini kuwa hakuna tatizo katika zoezi la uhakiki wao na ni muhimu sana kujihakiki ili kujiwekea mazingira mazuri ya kufanya kazi zao kwa uhuru na uwazi.

“ Niwahakikishie wadau wetu kuwa zoezi hili ni muhimu sana kwenu na kwetu pia katika namna ya kuboresha utendaji kazi wetu,” alisema Bw. Katemba.

Naye Katibu wa Baraza la Mashirika yasiyo ya Kiserikali nchini Bw. Ismail Suleiman ameishukuru Serikali kuwa kuandaa na kuratibu zoezi la uhakiki wa mashirika hayo na kuwaomba wamiliki wa mashirka yasiyo ya kiserikali nchini kujitokeza kuhakiki mashirika yao.

“Niwaombe wamiliki wa Mashirika yasiyo ya kiserikali nchini tuendelee kujitokeza kwa wingi tuje tuhakiki mashirika yetu ili tuondokane na usumbufu mara baada ya kumalizika kwa kuda wa uhakiki ulioongezwa,” alisema Bw. Ismail.

Zoezi la uhakiki wa Mashirika Yasiyo ya Kiserikali nchini lilizinduliwa na katibu Mkuu Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Agosti 21,2017 na uhakiki huo ulitekelezwa kwa muda wa wili mbili mpaka Septemba 04,2017.

Hata hivyo kutokana na sababu za kijiografia na mwitikio mkubwa wa mashirika kutaka kuhakikiwa ikaamuliwa kuongeza kwa muda wa siku 16 mpaka Septemba 20 mwaka huu, ambao ndio utakuwa mwisho wa uhakiki.

No comments:

Post a Comment