Sunday, August 13, 2017

Usain Bolt aumia na kushindwa mbio zake za mwisho mashindano ya dunia ya IAAF


Usain Bolt
Usain Bolt aliumia na kushindwa kumaliza mbio zake za mwisho za ubingwa wa dunia jijini London, na mwanariadha mwenzake Yohan Blake anasema huenda kucheleweshwa kwa mbio hizo kulimwathiri.
Bolt alipata mkakamao wa misuli na kulazimika kuondoka uwanjani alipokuwa akikimbia mbio za kupokezana vijiti za 4x100m ambazo timu ya Uingereza ilishinda.

Yohan Blake alisema hilo: "Mbio zilicheleweshwa dakika 10, tuliwekwa tukisubiri kwa dakika 40. Ilitushangaza sana.
"Watuweka muda mrefu sana tukisubiri."
Bolt alikuwa ametumai kwamba angemaliza maisha yake ya ukimbiaji kwa kushinda dhahabu mbili mashindano hayo ya London lakini ameondoka sasa na nishani ya shaba pekee aliyoishinda kwenye mbio za mita 100 wikendi iliyopita.

Sekunde chache baada yake kupokezwa kijiti awamu ya mwisho ya mbio hizo, alitatizima na kuanguka sakafuni.
Daktari wa timu ya Jamaica Kevin Jones amethibitisha kwamba Bolt alipatwa na mkakamao wa misuli ya mguu wake wa kushoto.
"Ilikuwa dakika 40 na walitoa nishani kwa washindi wa mbio mbili kabla yetu kukimbia," aliongeza bingwa wa zamani wa mbio za mita 100 Blake.
"Tulikaa tukipasha misuli joto na kusubiri, kisha tunapasha misuli moto tena na kusubiri. Nadhani hilo lilitwathiri.
"Inauma kumuona jagina halisi, bingwa halisi akiingia uwanjani na kutatizika kwa namna hiyo."
Bingwa wa mbio za 110m za kuruka viunzi Omar McLeod, aliyeongoza timu ya Jamaica ambayo ilikuwa imeshinda ubingwa wa mbio za 4x100m katika makala manne yaliyopita ya ubingwa wa dunia, alikubaliana na mtazamo wa Blake.
Usain Bolt
Sherehe za kumuaga Mo Farah baada yake kumaliza nafasi ya pili mbio za 5000m zilionekana kuchelewesha ratiba, na pia Farah alikabidhiwa nishani yake kabla ya fainali ya mbio hizo za kupokezana vijiti.
"Inauma sana. Nilijitolea kabisa na nilitaka sana kumuona Usain akiondoka kwa ushindi, au hata kama ingekuwa nishani tu. Inashangaza bwana, tulisubiri muda mrefu. Nilikunywa chupa mbili za maji.
"Lakini jina la Usain Bolt litasalia kukumbukwa."
Mshindi wa mbio za 100m Justin Gatlin alisema Bolt 'ndiye bado bora zaidi duniani' baada yake kushinda nishani ya fedha na timu yake ya Marekani.
Usain Bolt
Alikiri kwamba huenda hali ya hewa ilimwathiri Bolt.
"Nafikiri ni hali ya hewa iliyomsababishia Bolt jeraha. Lakini bado ndiye bora zaidi duniani. Huu ni wakati wa kuaga, naanza kumkosa tayari. Sehemu ya kupashia misuli moto, huwa tunaheshimiana na tulisalimiana. Usain Bolt ni mwanariadha mzuri sana."
 
Nishani alizoshinda Usain Bolt
2007 Ubingwa wa Dunia Fedha (200m), Fedha (4x100m kupokezana vijiti)
2008 Olimpiki Dhahabu (100m), Dhahabu (200m)
2009 Ubingwa wa Dunia Dhahabu (100m), Dhahabu (200m), Dhahabu (4x100m kupokezana vijiti)
2011 Ubingwa wa Dunia Dhahabu (200m), Dhahabu (4x100m relay)
2012 Olimpiki Dhahabu (100m), Dhahabu (200m), Dhahabu (4x100m kupokezana vijiti)
2013 Ubingwa wa Dunia Dhahabu (100m), Dhahabu (200m), Dhahabu (4x100m kupokezana vijiti)
2015 Ubingwa wa Dunia Dhahabu (100m), Dhahabu (200m), Dhahabu (4x100m kupokezana vijiti)
2016 Olimpiki Dhahabu (100m), Dhahabu (200m), Dhahabu (4x100m kupokezana vijiti)
2017 Ubingwa wa Dunia Shaba (100m)

No comments:

Post a Comment