Friday, June 8, 2018

Mfumuko Wa Bei Nchini Waendelea Kupungua Toka Asilimia 3.8 Hadi Asilimia 3.6

Na. Eliphace Marwa – Maelezo
Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS) leo imetoa taarifa ya mfumuko wa bei kwa mwezi Mei mwaka huu ambao umepungua hadi kufikia asilimia 3.6 ikilinganishwa na asilimia 3.8 ilivyokuwa kwa mwezi Aprili mwaka huu.

Akizungumza na waandishi wa habari Mkurugenzi wa Sensa ya Watu na Takwimu za Jamii kutoka Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS), Ephraim Kwesigabo amesema kuwa kupungua kwa bei kumechangiwa sana na kupungua kwa mfumuko wa bei za bidhaa za vyakula.

“ Baadhi ya bidhaa za chakula zilizochangia kupungua kwa mfumuko wa bei ni pamoja na mahindi kwa asilimia 10.3, unga wa mahindi kwa asilimia 12.5, mtama kwa asilimia 13.8, unga wa mihogo kwa asilimia 15.2, viazi mviringo kwa asilimia 9.0 na mihogo mibichi kwa asilimia 12.6, alisema bwana Kwesigabo.

Aidha ameongeza kuwa kasi ya mabadiliko ya bei za bidhaa na huduma kwa mwaka ulioishia mwezi Mei, 2018 imepungua ikilinganishwa na kasi ilivyokuwa kwa mwaka ulioishia mwezi Aprili 2018.

Hali ya mfumuko wa bei kwa baadhi ya nchi za Afrika Mashariki kwa mwaka ulioishia mwezi Mei, 2018 nchini Uganda umepungua hadi asilimia 1.7 kutoka asilimia 1.8 kwa mwaka ulioishia mwezi aprili 2018.

Aidha kwa upande wa Kenya mfumuko wa bei kwa mwaka ulioishia mwezi Mei, 2018 umeongezeka kidogo hadi asilimia 3.95 kutoka asilimia 3.73 kwa mwaka ulioishia mwezi Aprili, 2018.

Mfumuko wa bei unapima kiwango cha kasi ya mabadiliko ya bei za bidhaa na huduma zote zinazotumiwa na kaya binafsi.

No comments:

Post a Comment