Thursday, November 30, 2017

Marekani yataka mataifa yote kukatiza uhusiano na Korea Kaskazini

Kiongozi wa Korea Kaskazini Kim Jong un na mwenzake wa Marekani Donald Trump
Marekani imeyataka mataifa yote kukatiza uhusiano wa kidiplomasia na ule wa kibiashara na Korea Kaskazini baada ya taifa hilo kufanyia jaribio la kombora lake la masafa marefu.

Akizungumza katika baraza la usalama la umoja wa kimataifa ,mjumbe wa Marekani katika baraza hilo Nikki Haley amesema kuwa rais Trump amemtaka mwenzake wa China kukata usambazaji wa mafuta kwa Pyongyang.
Amesema kuwa Marekani haitaki mzozo lakini Korea Kaskazini itaangamizwa iwapo vita vitazuka.
Onyo hilo linajiri baada ya Pyonyang kufanyia majaribio kombora lake la kwanza katika kipindi cha miezi miwili.

Korea Kaskazini imesema kuwa kombora hilo lililorushwa siku ya Jumatano ambalo inasema liliruka kimo cha kilomita 4,475, ikiwa ni mara kumi zaidi ya kimo cha kituo cha angani.
Madai hayo hayakuthibitishwa na wataalam wametiliashaka uwezo wa taifa hilo kuwa na teknolojia kama hiyo.
Hatahivyo kiongozi wa Korea Kaskazini Kim Jong Un amesema kuwa uzinduzi wa kombora hilo ulikuwa wa kufana.
Jaribio hilo likiwa mojawapo ya majaribio yaliofanywa na taifa hilo limeshutumiwa na jamii ya kimataifa na tayari baraza la usalama la umoja wa kimataifa limeitisha kikao cha dharura.
Bi Haley alionya kuwa kuendelea kwa uchokozi kunalenga kuliyumbisha eneo hilo.
''Tunahitaji China kuchukua hatua zaidi'', alisema.
Rais Trump alimpigia simu rais Xi Jinping mapema siku ya Jumatano , Ikulu ya Whitehouse ilisema kuwa rais Trump alizungumza na Xi Jinping kwa simu akimtaka kuchukua hatua zozote kuishawishi Korea Kaskazini kusitisha uchokozi na kusitisha mpango wake wa kinyuklia.

No comments:

Post a Comment