Wednesday, April 25, 2018

Polisi Dar Yatoa ONYO Kwa Waliopanga Kuandamana

Jeshi la Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam limewataka wananchi wote kuendelea na shughuli zao kama kawaida kwa kuwa maandamano yanayozungumzwa hayapo na ni batili.

Akizungumza leo Jumatano Aprili 25 na shirikisho la waendesha bodaboda Mkoa wa Dar es Salaam, Kaimu Kamanda wa Polisi Kanda Maalum, ACP Sweethbert Njwele amesema jeshi la polisi limejipanga kuhakikisha kila mtu anafanya shughuli zake kama kawaida bila uvunjifu wowote wa amani.

"Niwahakikishie jeshi la polisi tumejipanga na mkoa wetu utaendelea kubaki salama hakuna maandamano yatakayofanyika hivyo kila mtu aendelee na shughuli zake kama kawaida," amesema Njwele.

Amesema waendesha bodaboda ni kundi kubwa ila kuna baadhi yao si waaminifu na kutaka wajiepushe na watu watakaowashawishi kuvunja sheria za nchi.

Kwa upande wake, Msemaji wa Shirikisho hilo Adamu Kyando amesema uvumi unaosambaa kwenye mitandao ya kijamii kuwa Aprili 26 bodaboda watashiriki si kweli kwani hakuna bodaboda yeyote atakayeshiriki maandamano hayo.

"Kuna taarifa zinazosambaa kwenye mitandao yakijamii ikihamasisha bodaboda kushiriki maandamano taarifa hizi si za kweli na ni batili," amesema Kyando.

Amesema kwa yeyote atakayeshiriki maandamano hayo uongozi hautahusika kwani taarifa zinazosambazwa hazitoki kwenye shirikisho hilo.
by richard shiyo/rich voice

No comments:

Post a Comment