Monday, October 23, 2017

JESHI LA POLISI LAKABIDHIWA MAGARI 18 YA KISASA YALIYOKUWA MABOVU.

Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam Mheshimiwa Paul Makonda jana Oktoba 22 amekabidhi Magari ya kisasa 18 kati ya 26 yaliyopelekwa Mkoani Kilimanjaro yakiwa Mabovu (Mkweche) kwaajili ya kufufuliwa upya.

Magari hayo yalipelekwa Kilimanjaro yakiwa yamebebwa kutokana na ubovu lakini sasa yanarejea Dar es Salaam
yakiwa Mazima na Mwonekano kama Magari ya UN ambapo yatakuwa na uwezo wa kubeba Askari 11 wakiwa wamekaa na silaha zao.
Akikabidhi Magari hayo kwa Jeshi la Polisi leo RC Makonda amesema yataenda kuhudumia Wananchi kwa kuimarisha Ulinzi na Usalama jijini Dar es Salaam.
 
Amesema kuwa kilichomgusa kuboresha Jeshi la Polisi ni Baada ya kuona Askari wakifanya kazi katika mazingira magumu na wakati mwingine kuvamiwa na majambazi kisha kuuawa na kuporwa Silaha.
Aidha RC Makonda ameishukuru kampuni ya Rajinder Motors Ltd (RSA) kwa kumuahidi kutengeneza Magari 56 ya Polisi Dar es Salaam bila kutumia fedha za serikali (Bure).
 
Makonda ametumia Makabidhiano hayo kutuma salamu kwa Majambazi, Vibaka na wale wenye nia ya kuvuruga Amani na Usalama kuwa kiama chao kimefika.
Amesema alipotangaza mpango wa kufufua Magari yaliyokufa wapo waliombeza lakini sasa wanajionea Magari yakiwa Mapya.
Makabidhiano hayo yameshuhudiwa pia na Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro Anna Mghwira, Kamanda wa Polisi kanda Maalumu ya Dar ea Salaam Lazaro Mambosasa na viongozi wengine wa vyombo vya Ulinzi na Usalama ambapo wamempongeza RC Makonda kwa ubunifu mkubwa alionao.

No comments:

Post a Comment