Tuesday, October 24, 2017

Tuzo za Mawaziri na Wabunge watakaofanya vizuri zazinduliwa

Wabunge na Mawaziri watakaofanya vizuri katika kutekeleza majukumu ya kuwaletea Wananchi maendeleo.

Hayo yamesemwa Jijini Dar es Salaam na Katibu wa Kamati hiyo Bw. Wilson Maage alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari, juu ya uzinduzi wa shindano hilo ambalo litafanyika kwa muda wa miezi miwili.

“Tuzo hizo zimetokana na kuwepo wazo bunifu (intellectual property) ambalo azma yake ni kuhamasisha utekelezaji wa shughuli za huduma na maendeleo kwa wananchi wa Tanzania na kupima kasi ya utekelezaji wa shughuli hizo kwa viongozi wa ngazi mbalimbali katika sekta na taasisi za kiserikali hapa nchini,” alifafanua Maage.

Aliendelea kusema kuwa, vigezo vitakavyotumiwa katika kuteua viongozi hao ambao ni wabunge pamoja na Mawaziri ni pamoja na kuwa mtetezi wa Wananchi wake bila uoga akiwa ndani au nje ya Bunge, mtendaji bora wa maendeleo yenye kuonekana, sifa ya kutoa hoja zenye tija kwa kutumia lugha ya staha bila matusi, sifa ya utekelezaji wa haraka apatapo matatizo ya Wananchi wake pamoja na sifa ya kutetea demokrasia, uhuru na kutetea wanyonge.

“Faida za shindano la tuzo hizi ni kwamba zinaweka Wananchi karibu na viongozi, kuchochea utekelezaji huduma na maendeleo kwa kasi ya juu, utawla bora na uwajibikaji wa viongozi kwa Wananchi, uhusiano mzuri kati ya serikali na Wananchi na kuimarisha furaha, utulivu na amani,” alieleza Maage.

Kwa upande wake Mkurugenzi mkuu wa Kamati hiyo, Herman Mnenuka alisema kuwa Wananchi ndiyo nguzo kuu ya kupata kiongozi atakayepata tuzo hiyo kwani wao ndio watakaopendekeza majina ya wabunge pamoja na mawaziri wanaofaa kuwania tuzo hiyo.

Katika tuzo hiyo, hatua ya kwanza, wananchi wanapaswa kupendekeza wabunge 15 kwa kila kigezo shindanishi, pia Wananchi watawateua Mawaziri 5 kwa kila kipengele shindanishi kwaajili ya kuingia kwenye ushindani wa tuzo hiyo na wabunge watano na Mawaziri watatu watakaopata kura nyingi kwa njia ya ujumbe mfupi (SMS) kutoka kwa wananchi wataingia katika fainali ya king’anyiro kuwania tuzo hiyo.

Aidha aliongeza kuwa, katika hatua nyingine, wananchi kupitia simu watawachuja washiriki waliofika hatua ya fainali kwa kutuma SMS na mbunge pamoja na waziri atakayepata kura nyingi ndiye atakaye kuwa mshindi katika kilele cha tuzo hiyo kitakachofanyika tarehe 23 Desemba Mwaka huu.

“Niwaombe wananchi washiriki kikamilifu ili kuweza kupata kiongozi anayejishughulisha na anayechapa kazi kupitia tuzo hii na mwisho wa kilele tutapata mshindi wa kila kipengele kilichowekwa ambacho kina tija muhimu katika taifa kupitia waheshimiwa wabunge na mawaziri wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,” alieleza Mnenuka.

Aidha aliongeza kuwa, Wananchi watapendekeza majina kwa kutuma ujumbe mfupi wa simu kupitia namba 15555 kwa mitandao ya Tigo, Airtel, Vodacom, Halotel Smart na Zantel na kila SMS itatozwa gharama ya shilingi 500 vilevile kutakuwa na vipindi vya radio runinga na magazeti ili kuwakumbusha mwenendo na hatua za shindano la tuzo za THSDA hadi siku ya kilele.

Hizi ni tuzo za kwanza kuandaliwa hapa nchini na kamati hiyo ambazo zitafanyika kwa awamu kulingana na upatikanaji wa rasilimali fedha.

No comments:

Post a Comment