Wednesday, June 19, 2019

POLISI WAMSHIKILIA KIJANA WA MIAKA 19 KWA TUHUMA ZA MAUAJI YA MWANAFUNZI JIJINI DAR

*

JESHI la Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam inamshikilia kijana mweye umri 19 Ernest Joseph kwa tuhuma za mauji ya mwanafunzi wa Chuo Kikuu cha Kimataifa cha Kampala (KIU) kilichopo Gongolamboto jijini Anifa Mgaya(21).
Kijana huyo anayetuhumiwa kufanya mauaji hayo tayari amekiri kuhusika na ameliambia Jeshi la Polisi kuwa baada ya kufanya tukio hilo la mauaji kwa kumchoma kisu kifuani upande wa kulia alichukua simu aina ya Tekno na fedha Sh.8000 ambazo zilikuwa kwenye pochi.

Akizungumza kukamatwa kwa mtuhumiwa huyo Kamanda wa Jeshi la Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam Lazaro Mambosasa amesema mtuhumiwa huyo amefanya tukio hilo la mauaji Juni 16 mwaka huu saa tatu usiku maeneo hayo ya Chuo cha Kampala.
"Mtuhumiwa amekiri kuhusika na mauaji ya mwanafunzi Anifa Mgaya (21) ambaye alikuwa anasoma chuoni hapo ngazi ya Diploma.Mtuhimiwa alimchoma kisu mwanafunzi huyo kifuani na kisha kuchukua simu ya Tekno na fedha Sh.8000.

"Mwanafunzi alifariki dunia muda mfupi baada ya kutokwa na damu nyingi, na mtuhumiwa alikimbia baada ya kutenda kosa hilo.Jeshi la Polisi tuliahidi kumsaka aliyehusika kokote aliko na jana tukamkata akiwa maeneo ya Madale Mivumonijijini Dar es Salaam,"amesema Kamanda Mambosasa.

Akifafanua zaidi kuhusu tukio hilo, Kamanda Mambosasa amesema katika mahojiano mtuhimiwa amekiri kumchoma kisu na kueleza namna ambavyo Anifa alikuwa amevaa siku hiyo kwa kueleza alikuwa amevaa fulana nyeusi , suruali ya jinsi na kapelo.
"Mtuhumiwa anaendelea kushikiliwa na atafikishwa mahakamani kujibu tuhuma zinazomkabili,"amesema Mambosasa na kuongeza kuwa Jeshi la Polisi liliahidi kumsaka mtuhumiwa aliyehusika na mauji ya mwanafunzi huyo kwani damu yake haijamwagika bure.

Wakati huo huo Kamanda Mambosasa amesema kuwa wakati wa msako huo , wamekamata wahalifu wengine 31 ambao wamekuwa wakifanya matukio ya uhalifu chuoni hapo na kusababisha hofu kwa wanafunzi, ambao Polisi imeeleza kuwa itaendelea kuwahoji watuhumiwa hao na kisha sheria ichukue mkondo wake.
Mambosasa amesema kuwa Jeshi la Polisi Kanda ya Dar es Salaam litaendesha msako kusaka wahalifu wote walioko kwenye maeneo ya vyuo na kufafanua yoyote ambaye anajihusisha na matukio ya uhalifu atachukuliwa hatua.

No comments:

Post a Comment