Wednesday, May 30, 2018

Walioshtakiwa ulaji rushwa Kenya kukaa rumande wiki moja

Mkurugenzi Mkuu wa NYS Richard Ndubai akiwa mahakamani Jumanne 
Watuhumiwa 24 walioshtakiwa kuhusiana na kashfa ya ufujaji wa pesa katika Shirika la Vijana wa huduma kwa Taifa (NYS) watakaa rumande kwa wiki moja.

Jaji ameamuru wazuiliwe hadi Jumatatu wiki ijayo ambapo uamuzi wa kuachiliwa kwa dahamana utatolewa.
Miongoni mwa walioshtakiwa jana ni Katibu Mkuu wa Wizara ya Vijana na Jinsia Lilian Mbogo Omollo na Mkurugenzi Mkuu wa shirika hilo Richard Ndubai.
Walikamatwa na wengine wakajisalimisha kwa polisi Jumatatu wiki hii na kisha kufikishwa kortini Milimani, Nairobi jana.
Kikao cha kusikizwa kwa kesi dhidi yao kiliendelea hadi usiku wa manane.
Upande wa mashtaka ulipinga washukiwa kupewa dhamana kwa misingi ifuatayo:

  • Lilian Omollo: Alikuwa katibu mkuu katika wizara ya utumishi kwa umma na masuala ya vijana na ya kijinsia na ndiye aliyekuwa ni afisa mhasibu wakati malipo hayo ya ulaghai yalipotolewa
  • Sammy Mbugua Mwangi: Mkuu wa hesabu katika wizara ya utumishi wa umma. Alikuwa mtu wa mwisho kuidhinisha malipo ya ulaghai kwa mabenki kupitia intaneti na alizilipia vocha kadhaa zisizokuwa na saini stahiki kama ilivyoshuhudiwa katika vocha zilizopatikana.
  • Micheal Ojiambo: Ni mkurugenzi wa usimamizi katika wizara na ndiye aliyewasilisha kwa katibu mkuu katika wizara, vocha za malipo ambazo hazikuwepo kwenye orodha ya uthibitisho wa kamati na kuziidhinisha kuwa sawa kama ilivyoshuhudiwa katika ilani za kuwasilisha vocha hizo.
  • Clement Murage: Alikuwa mhasibu mkuu wa zamani aliyekuwa na jukumuu kuu katika utoaji wa malipo hayo ya ulaghai aliyesaini kuidhinisha malipo kwa vocha na alikuwa mmojawapo ya wanakamati ya pili ya uthibitisho na hakuthibitisha uhalisi wa malipo hayo ya ulaghai ya vocha.
  • Richard Ethan Ndubai:Ni mkurugenzi mkuu wa shirika la NYS na ndiye aliyesaini kuidhinisha malipo hayo ya ulaghai.
Upande wa mashtaka ulikuwa umepinga kuachiliwa kwao ukisema wanaweza kutoroka au kukosa kurejea mahakamani wakati wa kusikizwa kwa kesi dhidi yao.

No comments:

Post a Comment