Wednesday, March 21, 2018

Kilichoendelea LEO baada ya IGP, AG na DCI kuitwa Mahakamani Kesi ya Nondo


Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, imepanga Aprili 4, 2018 kusikiliza maombi ya Mwenyekiti wa Mtandao wa Wanafunzi (TSGN), Abdul Nondo.

Nondo ambaye ni mwanafunzi wa mwaka wa tatu katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) amepandishwa kizimbani katika Mahakama ya Iringa.

Uamuzi huo umetolewa leo Machi 21, 2018 na  Jaji  Rehema Samuje wakati shauri hilo lilipofikishwa mahakama hapo kwa ajili ya kutajwa.

Hatua hiyo inatokana na Mtandao wa Watetezi wa Haki za Binadamu(THRDC), Kituo  cha Sheria na Haki   za Binadamu(LHRC) na Mtandao wa Wanafunzi Tanzania(TSNP) kuomba mambo matatu ikiwemo Nondo kupewa dhamana.

Jaji Sameja ameutaka upande wa Jamhuri kujibu hoja za utetezi dhidi ya Nondo, Machi 26, 2018.

“Kesi ya msingi itakuja kusikilizwa April 4 lakini upande wa Jamhuri mnatakiwa kuja kujibu hoja za upande wa wawasishaji maombi,” alisema Jaji Sameja.

“Pia upande wa wawasilishaji maombi mnapaswa kuwasilisha maombi ya nyongeza Machi 27, mwaka huu.”

Machi 19, 2018 THRDC, LHRC na TSNP  waliwasilisha maombi namba 49, 2018  Mahakama Kuu kutaka itoe amri kwa Jeshi la Polisi kumpeleka mahakamani Nondo.

Wakili wa Nondo, Jebra Kambole  amedai maombi hayo yalifunguliwa dhidi ya Mkurugenzi wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai (DCI) Mkuu wa Jeshi la Polisi (IGP) na Mwanasheria Mkuu wa Serikali ambapo wapeleka maombi wanaiomba mahakama kutoa amri ya kuletwa mahakamani kwa mwanafunzi Nondo au kumuachia kwa dhamana kwani ameshikiliwa na polisi kwa muda mrefu bila sababu za msingi kutolewa.

Hata hivyo, kwa sasa Nondo amenyimwa dhamana na mahakama mjini Iringa ambayo inataka kujiridhisha na usalama wake.

No comments:

Post a Comment