Tuesday, March 6, 2018

Mkapa amteua Prof. Mubofu kuwa Makamu Mkuu wa chuo cha Dodoma (UDOM) Kuchukua Nafasi ya Profesa Kikula

Na Paschal Dotto-MAELEZO    
Mkuu wa Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM) Rais Mstaafu (Awamu ya Tatu), Mhe. Benjamin William Mkapa ametangaza uteuzi wa  Profesa Egid Beatus Mubofu kuwa Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu hicho, nafasi iliyokuwa inashikiliwa na Profesa Idris Suleiman Kikula.

Uteuzi huo umetangazwa rasmi  tarehe 5, Machi 2018 kupitia taarifa iliyotolewa kwa vyombo vya habari na ofisi   ya Mkuu wa UDOM, Mhe. Benjamin Mkapa.

Kabla ya uteuzi huo Profesa Mubofu alikuwa Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Viwango Tanzania (TBS), na kabla ya hapo alikuwa Mhadhiri Mwandamizi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM).

Kwa mujibu wa taarifa hiyo, uteuzi wa Profesa Mubofu unaanza rasmi tarehe 17 Machi, 2018.

Profesa Idris Kikula ni miongoni mwa wanazuoni waandamizi wanaoheshimika ndani  na nje ya nchi kitaaluma kwa kushiriki katika tafiti mbalimbali za kisayansi na kijamii

Ameshiriki katika tafiti hizo kwa kushirikiana na taasisi nguli za kitafiti hapa nchini  kama REPOA, pamoja na taasisi ya UONGOZI.

UDOM ndio chuo kikuu pekee chenye uwezo mkubwa wa kuchukua wanafunzi wengi hapa nchini na Afrika Kusini mwa jangwa la Sahara na inakadiriwa kina uwezo wa kuchukua wanafunzi takriban 40,000, pia kina eneo la ukubwa wa hekari zaidi ya 6000.

No comments:

Post a Comment