Tuesday, March 6, 2018

Rais Magufuli atoa kibali cha kuendelezwa ujenzi wa msikiti wa Sumbawanga......Serikali ya mkoa wa Rukwa yachangia Milioni 5.7 kuumalizia

Uongozi wa Waislamu Mkoani Rukwa umepokea kwa furaha mchango wa Shilingi Milioni 5.7 uliotolewa na uongozi wa serikali ya Mkoa wa Rukwa ukiongozwa na Mkuu wa mkoa wa Rukwa Mh. Joachim Wangabo katika kikao cha maridhiano juu ya ujenzi wa msikiti uliosimama kwa muda.

Fedha hizo zilizochangwa zilijumuisha ahadi, fedha taslimu pamoja na vifaa vya ujenzi vilivyotolewa kwa umoja wa viongozi wa serikali kuonesha mshikamano uliopo kati ya serikali na wananchi bilaya kujali itikadi, dini wala rangi huku Mh. Wangabo akichangia milioni 1.5

Kabla ya maridhiano hayo Mh. Wangabo alitoa salamu za rais Dk. John Pombe Magufuli juu ya kuuendeleza msikiti huo na kunukuu kuwa Mheshimiwa Rais ametoa kibali cha kuuendeleza msikiti hio na yupo tayari kuweka jiwe la msingi ama kuuzindua msikiti huo.

“Mh. Rais ameniagiza niseme yafuatayo kuwa ametoa kibali cha kuendelea kujenga msikiti huu ahdi umalizike, ameyafikiria mambo mengi sana mpaka kuja kufikia maamuzi haya, ili yalete muskabali wa maridhiano, ilete amani, ilete utulivu, mshikamano, maoelewano na umoja ili Rukwa yetu iweze kusonga mbele kama kitu kimoja., la pili alisema kuwa yupo tayari kuweka jiwe la msingi ama la kuzindua msikiti huu,”

Kwa kuongezea hilo Mh. Wangabo aliuomba uongozi wa uislamu mkoa kuendelea kushirikiana na kudumiasha amani na kuhakikisha wanajenga Rukwa moja isiyoyumbishwa na tofauti yoyote kwani ushirikiano huo umekuwa wa muda mrefu hovyo asingependa pawepo na tofauti.

Pia alimuagiza Mkurugenzi wa Manispaa ya Sumbawanga kuhakikisha vikwazo vyote vianondolewa na kumtaka kamishna wa ardhi nyanda za juu kusini kufanya haraka kupitisha kibali ili msikiti huo upatiwe hati.

Kwa upande wake Shekhe Mkuu wa mkoa wa Rukwa Rashid Akilimali amesifu maamuzi ya Rais Dk. John Pombe Magufuli na kukubali ombi lake la kutaka kuja kuweka jiwe la msingi ama kuuzindua msikiti huo na kuwa waislamu wataendelea kuungana nae na kumuombea amalize vipindi vyake salama.

“Mh. Mkuu wa Mkoa kwa niaba ya waislamu wa mkoa wa Rukwa kwanza tunatoa shukrani za dhati kwa Mh.Rais wa nchi Mh. Dk. John Magufuli, nimeamini kama alivyosema kuwa yeye ni msikivu na yeye anatuomba kila siku tumuombee dua na sisi mwisho wa khotuba yetu kila ijumaa tunadua huwa tunaiomba, Eee Mola wetu linda amani ya nchi yetu na uwalinde viongozi wetu,” Shekh Akilimali alimalizia.

Uongozi wa mkoa wa Rukwa uliowajumuisha kamati ya ulinzi na usalama ya Mkoa, Wakuu wa Wilaya, Mkurugenzi wa halmashauri, Mbunge wa jimbo la Sumbawanga mjini, Mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Sumbawanga pamoja na kaimu Kamishna wa Ardhi nyanda za juu kusini.

No comments:

Post a Comment