Wednesday, January 17, 2018

RC Makonda amfuta machozi mjane ambaye nyumba yake iliuzwa na matapeli

Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam Paul Makonda amemsaidia mama mjane Benadetha Rwendela aliedhulumiwa nyumba yake Plot No. 239 Block B Kunduchi Beach kwa kupigwa mnada na madalali kutoka kampuni ya Nkanya Ltd kinyume na taratibu kisha kuamrishwa kuondoka ndani ya siku 30.


Baada ya RC Makonda kuona taarifa hizo kwenye baadhi ya vyombo vya vabari na mitandao alimuita mjane huyo ofisini kwake kisha kumkutanisha na wanasheria wa mkoa na kubaini utapeli mkubwa uliotumika kuuza nyumba hiyo kutokana na watu kufoji nyaraka ikiwemo sahihi ya mwenyekiti wa mtaa huku nyumba hiyo ikiwa na zuio la Mahakama.

Aidha imebainika kuwa hati za nyumba hiyo zilifojiwa kisha kutumika kuchukuwa mkopo wa shilingi bilioni moja pasipo mmiliki wa nyumba kujua kinachoendelea.

Kutokana na hilo RC Makonda ameagiza Kamanda wa Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam Lazaro Mambosasa kuwakamata matapeli waliohusika pamoja na kuagiza kusimamishwa mnada huo kwakuwa ni batili huku akimsihi mama mjane kuishi kwa amani kwenye nyumba yake.

Aidha RC Makonda amesema Jumatatu ya wiki ijayo atakutana na Bank ya KCB kwa ajili ya mazungumzo huku akiwaagiza madalali wote wanaotaka kufanya minada kwenye mkoa huu kuhakikisha wanapata ruhusa kutoka kwa wakuu wa wilaya.

Kwa upande wake mjane huyo Benadetha Rwendela ameishukuru Serikali ya awamu ya tano kwa kuwajali wananchi wake na kuwasaidia pale wanapopata matatizo huku akimpongeza Rais Magufuli kwa kumteua RC Makonda.

No comments:

Post a Comment