Sunday, January 7, 2018

WAZIRI MPINA AKAMATA KILO 65,600 ZA SAMAKI ZENYE THAMANI YA SHILINGI MILIONI MIA TATU

Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Luhaga Joelson Mpina amekamata kilo 65600 za samaki wachanga aina ya Sangara waliokaushwa kwa chumvi wenye thamani ya shilingi milioni mia tatu katika Kisiwa cha Lubili wilayani Muleba kwenye Mkoa wa Kagera baada ya wamiliki wa samaki hao kukimbia.
Akizungumza leo na Waandishi wa Habari katika Ofisi ya Kitengo cha Doria na Udhibiti wa Uvuvi wa mpakani katika Mkoa wa Kagera, Mpina amesema tukio la kukamatwa kwa samaki hao lilifanikiwa baada kupata taarifa kutoka kwa raia
mwema ambapo aliagiza mamlaka za Wilaya ya Muleba kufuatilia kwa karibu hatimaye kuwakuta samaki hao wakiwa wameanikwa chini katika kisiwa hicho.

Waziri Mpina amesema Sheria ya Uvuvi namba 22 ya Mwaka 2003 na Kanuni zake za mwaka 2009 kifungu cha 90(1) inataka samaki wanaovuliwa waandaliwe katika mazingira yanayokidhi vigezo vya usalama kwa mlaji na kwamba ni kosa kisheria kuwavua au kuchakata samaki aina ya Sangara walio chini ya sentimeta 50 kwa kuwa ni wachanga na sentimita 25 kwa Samaki aina ya Sato. Pia sentimita 85 kwa Sangara kwa kuwa ni wazazi wanaotakiwa kundelea kuzaa.

Waziri ameongeza kuwa Sheria hiyo imetoa mamlaka kwa watendaji wa Serikali kutaifisha mali zote zilitumika katika uvuvi haramu kupitia kifungu cha 37(a) (ii) na (iii) pamoja na Sheria ya Hifadhi za Bahari na Maeneo Tengefu namba 29 ya mwaka 1994.

Aidha Waziri Mpina ameagiza watendaji kufuata taratibu zote za kisheria ili samaki hao wauzwe kwa njia ya mnada na mapato hayo yaingie Serikalini mara moja.Aidha aliwaonya wafanyabiashara na wavuvi kuachana na uvuvi haramu kwa kuwa ni kuhujumu raslimali za taifa ambazo zingetumika kwa kizazi cha sasa na baadaye.

No comments:

Post a Comment