Thursday, February 15, 2018

Afrika Kusini: Ramaphosa kuapishwa kuwa rais

Cyril Ramaphosa 
Mwenyekiti wa chama tawala cha ANC Cyril Ramaphosa anatarajiwa kuapishwa kuwa rais wa Afrika Kusini baada ya rais wa taifa hilo Jacob Zuma kujiuzulu.
Bwana Zuma alikuwa chini ya shinikizo kali kutoka kwa chama chake cha ANC kilichomtaka ajiuzulu la sivyo akabiliwe na kura ya kutokuwa na imani dhidi yake bungeni.
Katika taarifa ya runinga, alisema kuwa anajiuzulu mara moja lakini hakubaliani na uamuzi wa chama.
Bwana Zuma anakabiliwa na madai kadhaa ya ufisadi lakini amekana kufanya makosa yoyote.
Akiwa naibu wa rais Ramaphosa anakuwa kaimu wa rais mara moja baada ya Zuma kujiuzulu.
Taarifa ya serikali inasema kuwa bunge litamchagua rais mpya wa Afrika Kusini Alhamisi jioni.
Bwana Zuma ,mwanachama wa jeshi la ANC wakati wa ubaguzi wa rangi, alipitia nyadhfa kadhaa za chama hicho hadi kuwa rais. 
Cyril Ramaphosa na Jacob Zuma
Aliliongoza taifa hilo kwa muda mrefu baada ya ubaguzi wa rangi.
Lakini anaachilia madaraka akikabiliwa na kashfa kadhaa huku uchumi wa Afrika kusini ukiwa katika hali mbaya.
Siku ya Jumatano, maafisa wa polisi walivamia nyumba ya Johanesburg ya familia ya Gupta iliokuwa na ushawishi mkubwa serikalini.
Familia hiyo imeshutumiwa kwa kutumia urafiki wao wa karibu na rais Zuma kujilimbikizia ushawishi mkubwa wa kisiasa .
Hatahivyo familia hiyo imekana hayo.

Nini kinafanyika sasa?

Kwa mujibu wa katiba , iwapo kutatokea pengo katika wadhifa wa rais, aliyeko chini ya wadhifa huo anakaimu urais:
(a) Naibu rais
(b) Waziri aliyechaguliwa na rais
(c) Waziri aliyechaguliwa na mawaziri wengine katika baraza
(d) Spika wa bunge, hadi bunge litakapomchagua mmoja wao kuchukuwa wadhifa huo.


Kama naibu rais, na pia mwenyekiti wa chama tawala ANC. Bwana Ramaphosa ndiye anayepokea wadhifa huo.
Licha ya taarifa za awali kwamba angependa kuchukuwa muda uliosalia kujitayarisha kwa uchaguzi wa mwakani, akiwa ndiye kaimu rais hivi sasa, anatarajiwa kuapishwa rasmi kama rais na bunge.

No comments:

Post a Comment