Thursday, September 7, 2017

Mtekaji Wa Watoto Arusha Auawa Kwa Kupigwa Risasi

Mtuhumiwa wa utekaji wa watoto Arusha, Samson Peter amefariki dunia kwa kupigwa risasi wakati akijaribu kuwakimbia Polisi alipokuwa amekwenda kuwaonyesha washirika wenzake wa utekaji eneo la Muriet Mkoni Arusha.

Akithibitisha kutokea kwa kifo chake Kamanda wa Polisi Mkoa wa Arusha Charles Mkumbo amesema kuwa mtuhumiwa huyo wa utekaji alipigwa risasi ya mguuni kama onyo la kujaribu kumtoroka Askari aliyekuwa ameongozana naye majira hayo ya saa 5:30 usiku.

Kamanda Mkumbo amesema kuwa baada ya tukio hilo la kumjeruhi  mtuhumiwa Samson Peter kwa nia ya kumuadhibu alifikishwa Hospital ya Mt. Meru lakini alifariki kutokana na kuvuja damu nyingi kwenye jeraha la mguu.

"Ni kweli mtuhumiwa amefariki. Ambapo jana usiku wakati alipokuwa amesindikizwa na polisi kuwaonyesha waashirika wenzake alitaka kutoroka, lakini katika hatua ya kumuadhibu kwa kitendo chake hicho ndipo akapigwa risasi ya mguuni ambapo ilimpelekea kuvuja damu nyingi na alifariki baada ya kufikishwa hospitali" amesema Kamanda Mkumbo.
 
Hata hivyo Kamanda Mkumbo amesema msako zaidi wa kuunasa mtandao huo bado unaendelea na iwapo wakipatikana wote watakumbana na mkono wa sheria.

No comments:

Post a Comment