Saturday, September 2, 2017

Uhuru Kenyatta: Sikubaliani na uamuzi wa Mahakama lakini Ntauheshimu


Rais wa Kenya, Uhuru Kenyatta amesema kuwa hakubaliani na uamuzi wa Mahakama ya Juu nchini humo ya kubatilisha uchaguzi wa urais uliopita na kuagiza kufanyika upya kwa uchaguzi lakini anaheshimu uamuzi huo wa mahakama.

Akizungumza na waandishi wa habari leo  kuhusu uamuzi huo wa Mahakama, Rais Kenyatta amesema kuwa Jubilee iko tayari kurejea kwenye uchaguzi kama Mahakama ilivyoamuru huku akiwataka Wakenya kudumisha amani.

“Wenzangu, amani… amani… amani. Mshike jirani yako mkono umwambie hii ni vita ya wale, sisi ni kitu kimoja. Sisi ni jamii ambayo inaitwa ‘Wakenya’ na hivyo ndivyo itakavyokuwa,” amesema Kenyatta.

“Na mimi namshukuru ndugu yangu hapa [Ruto] amesema yuko tayari kurudi uwanjani,” ameongeza.

Kenyatta amewataka Wakenya kujiandaa na uchaguzi mwingine na kwamba Jubilee wataingia tena barabarani ‘kupiga debe’ ili wachaguliwe tena.

Leo, Mahakama ya Juu iliamua kubatilisha uchaguzi wa Rais uliofanyika Agosti 8 mwaka huu ambao kwa mujibu wa Tume Huru ya Uchaguzi ya nchi hiyo, Kenyatta alishinda kwa zaidi ya asilimia 54 dhidi ya Raila Odinga (NASA) aliyepata asilimia 44.7.

Mahakama imeeleza kuwa kulikuwa na vitendo vya ukiukwaji wa sheria na katiba ya nchi hiyo uliopelekea uchaguzi huo kutofaa kuwa halali. Imeamuru uchaguzi huo kufanyika baada ya siku 60 (Novemba Mosi).

No comments:

Post a Comment