Friday, August 18, 2017

MAKAMU WA RAIS AWASILI NCHINI AFRIKA KUSINI KUMUWAKILISHA RAIS DKT. MAGUFULI KATIKA MKUTANO WA 37 WA SADC.

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan amewasili nchini Afrika ya Kusini tayari kwa kuhudhuria Mkutano wa 37 wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Jumuiya ya Maendeleo ya Kusini mwa Afrika SADC unaoaanza tarehe 19 na 20 ambapo kesho tarehe 18 atahudhuria Mkutano wa Dharura wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Troika Mbili ya SADC (SADC Double Troika Summit).


Mheshimiwa Makamu wa Rais Samia Suluhu Hassan amepokelewa na Waziri wa Mawasiliano wa Afrika Kusini Mhe. Ayanda Dlodlo, akimuwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt.John Pombe Magufuli
Akizungumza mara baada ya kuwasili kwa Makamu wa Rais, Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Dkt. Augastine Mahiga amesema Mkutano huo utapokea na kujadili ajenda mbalimbali ikiwemo uchaguzi wa Mwenyekiti na Makamu Mwenyekiti wa SADC na Uchaguzi wa Mwenyekiti na Makamu Mwenyekiti wa Asasi ya SADC ya Ushirikiano wa Siasa, Ulinzi na Usalama; Hali ya Michango mbalimbali ya Nchi Wanachama na Kupokea taarifa ya Mwenyekiti anayeondoka wa SADC Organ. 
Pia Mkutano utapokea taarifa ya Katibu Mtendaji wa SADC; Kupitia hali ya kiuchumi katika Kanda ya SADC; Kuwasilisha Kaulimbiu ya Mkutano wa SADC; Taarifa kuhusu Mfuko wa Maendeleo wa SADC; Taarifa ya Utekelezaji wa Mpango Mkakati wa Viwanda; Kuwezesha Chuo cha Elimu ya Sayansi na Teknolojia; Maombi ya Serikali ya Comoro na Serikali ya Burundi kujiunga na SADC; Utekelezaji wa Mabadiliko ya Kitaasisi ya Umoja wa Afrika na Mkutano wa Mshikamano kati ya SADC na Saharawi ya Magharibi. Dkt. Mahiga amesema katika Mkutano wa Dharura wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Troika Mbili ya SADC (SADC Double Troika Summit) Tanzania itakabidhi nafasi ya Uenyekiti kwa Mwenyekiti mpya.Double Troika inahusisha nchi wanachama sita ambao kwa sasa ni Swaziland, Tanzania, Afrika Kusini, Angola, Botswana na Msumbiji. Katika mkutano huo Mfalme Mswati III wa Swaziland atakuwa ndiye Mwenyekiti. 
Ajenda kuu katika Mkutano huu ni kupokea na kujadili taarifa kuhusu hali ya kisiasa, kiulinzi na kiusalama katika Kanda na hasa nchini DR Congo na Lesotho.

No comments:

Post a Comment