Saturday, August 26, 2017

Rais Magufuli afanya ziara ya kushtukiza Feri Dar na kutoa maagizo kwa RC Makonda


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli  tarehe 25 Agosti, 2017 amefanya ziara ya kushtukiza katika eneo la Feri na kisha kuvuka bahari kwa kutumia kivuko cha MV Kigamboni ambako amekutana na wananchi wa Kigamboni, ametembelea Chuo cha Kumbukumbu ya Mwl. Nyerere na ametembelea Daraja la Nyerere Jijini Dar es Salaam.

Baada ya kukata tiketi yake Mhe. Rais Magufuli alipata wasaa wa kuzungumza na wananchi aliosafiri nao katika kivuko cha MV Kigamboni na baadaye kuzungumza na wananchi wa Kigamboni ambapo ameulizwa na kujibu mambo mbalimbali.

Kuhusu ubovu wa barabara Mhe. Rais Magufuli alisema Serikali imechukua hatua ya kukabiliana  na tatizo hilo kwa kuanzisha Wakala wa Barabara Vijijini na Mijini (TARURA) ambayo itafanya kazi ya kutengeneza barabara kwa kiwango cha lami.

Kuhusu tatizo la kukatika kwa umeme alisema Serikali inatekeleza miradi mbalimbali itayoongeza kiwango cha umeme katika gridi ya taifa pamoja na kurekebisha miundombinu yake na amewaomba kuwa na subira wakati juhudi hizo zinaendelea.

Akiwa katika Chuo cha Kumbukumbu ya Mwl. Nyerere Mhe. Rais Magufuli alikutana na vijana wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) kutoka vyuo na vyuo vikuu vya Mkoa wa Dar es Salaam waliopiga kambi katika chuo hicho, ambao wamempongeza kwa kazi kubwa na nzuri anayoifanya kuiongoza Serikali ya Awamu ya Tano ambayo kwa muda mfupi imeonesha uongozi unaoacha alama.

Vijana hao walimhakikishia kuwa wanamuunga mkono na wamemuahidi kuwa wapo tayari kuitumikia nchi kwa jukumu lolote watakalopewa na kwamba daima watatanguliza maslahi ya nchi.

Akizungumza na vijana hao Mhe. Rais Magufuli aliwapongeza kwa moyo wa uzalendo waliouonesha, na amewataka kuwa nguzo imara ya mabadiliko ya kweli nchini ili juhudi zinazofanywa na Serikali ya Awamu ya Tano kurekebisha mambo yaliyosababisha kukiuka misingi ya Waasisi wa Taifa zizae matunda.

Mhe. Rais Magufuli alieleza baadhi ya juhudi hizo kuwa ni kukabiliana na rushwa inayodhohofisha uchumi na huduma za kijamii, kudhibiti mianya ya matumizi mabaya na upotevu wa fedha na mali za umma, kuondoa watumishi hewa na wenye vyeti vya kughushi, kuongeza bajeti ya maendeleo katika bajeti ya Serikali, kuongeza uzalishaji wa umeme, kujenga viwanda, kujenga reli, kununua ndege za Serikali, kuongeza ukusanyaji wa kodi na kuchukua hatua kali dhidi ya wahujumu uchumi.

“Nataka niwahakikishie vijana wote kuwa nawapenda sana, hata mimi nilikuwa Umoja wa Vijana, yote yaliyotokea kinyume na misingi ya chama hiki na misingi ya waasisi wetu wakiongozwa Hayati Mwl. Julius Kambarage Nyerere nimeamua kuyanyoosha na yatanyooka, na nyinyi simameni imara, kitumikieni chama na msitumikie watu au vikundi vya watu, mkifanya hivyo kila kitu kitakwenda vizuri kabisa” alisisitiza Mhe. Rais Magufuli.

Mhe. Rais Magufuli aliwataka vijana hao kujitokeza kugombea nafasi mbalimbali za uongozi katika uchaguzi wa chama utakaofanyika baadaye mwaka huu, na amebainisha kuwa wasiwe na hofu ya kuwepo kwa rushwa kwa kuwa wote watakaojihusisha na vitendo vya rushwa hawatapitishwa kuwania nafasi za uongozi ndani ya chama.

Pia aliwaambia viongozi wa Secretarieti ya CCM aliowakuta wakizungumza na vijana hao kuwa anazo taarifa zote juu ya watu waliojimilikisha mali za chama na amesema anasubiri wakati ukifika achukue hatua zinazostahili.

Baada ya kuzungumza na vijana hao Mhe. Rais Magufuli alitembelea Daraja la Nyerere na kuzungumza na wananchi wa eneo hilo, ambapo alimuagiza Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam Bw. Paul Makonda kufanyia kazi ombi la wananchi kujengewa kituo cha Daladala.

Gerson Msigwa
Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais, IKULU
Dar es Salaam
25 Agosti, 2017

No comments:

Post a Comment