Saturday, July 29, 2017

Mahakama Yaamuru Harbinder Singh Sethi Akatibiwe Muhimbili


Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu imeamuru mshtakiwa, Harbinder Singh Sethi apelekwe katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili (MNH) kwa ajili ya kupata huduma ya matibabu.

Hakimu Mkazi Mkuu, Huruma Shaidi alitoa amri hiyo jana  Ijumaa Julai 28 baada ya Sethi kuieleza mahakama hiyo kuwa hali yake kiafya bado ni mbaya na kwamba aliongea  na Magereza ili aweze kupata tiba toka kwa daktari wake, wakampeleka katika Hospitali ya Amana.

Amedai kuwa kutokana na maradhi yanayomkabili kuhitaji mtaalam ameshindwa kupata matibabu, hivyo ameomba asinyimwe haki ya kupata matibabu.

Baada ya kutolewa maelezo hayo, Mwendesha Mashtaka wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru), Vitalis Peter alieleza kuwa ni kweli mshtakiwa ameieleza mahakama kuhusu hali yake lakini hakuna nyaraka zinazounga mkono kutoka kwa mtaalam kuelezea hali yake.

Amebainisha kwa kuwa kutibiwa ni haki yake na kuwa wapo madaktari katika Hospitali ya Taifa  ya Muhimbili na Magereza.

Hakimu Shaidi alisema kusiwekwe kikwazo chochote kuhusu afya ya mshtakiwa hivyo aliamuru Magereza kumpeleka Muhimbili kwa ajili ya matibabu na tarehe ijayo watoe taarifa kama amri aliyoitoa imetekelezwa.

Upelelezi wa kesi hiyo hadi sasa haujakamilika na kesi imeahirishwa hadi Agosti 3, 2017 kwa ajili ya kutajwa ili kuangalia kama upelelezi utakuwa umekamilika ama la.

Awali, Julai 14, 2017, wakili wa Sethi, Alexi Balomi aliifahamisha mahakama kuwa Sethi anaumwa na hali yake imeendelea kuwa mbaya na alikuwa hawezi kupata usingizi kwa wiki nne.

Wakili Balomi aliiambia mahakama kuwa Sethi anasumbuliwa na uvimbe tumboni wenye ukubwa kama  puto ambao unahitaji uangalizi wa karibu wa madaktari wataalam na kwamba anahitaji uangalizi wa karibu wa madaktari.

Katika kesi hiyo, Sethi na James Rugemarila wanakabiliwa na mashtaka 12 ya uhujumu uchumi kwa kula njama, kujihusisha na mtandao wa uhalifu, kutoa nyaraka za kughushi, kujipatia fedha kwa njia za udanganyifu, kutakatisha fedha na kuisababishia Serikali hasara ya Sh 309 bilioni.

No comments:

Post a Comment